NA MWANDISHI WETU, LONGIDO
Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido limependekeza Mpango na Bajeti ya Halmashauri kuanzia Mwaka wa Fedha 2026/2027 kutoa kipaumbele katika ukamilishaji wa miradi viporo katika kila kijiji badala ya kuanzisha miradi mipya.
Hayo yameelezwa leo Februari 6, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Kudhibiti UKIMWI, Mhe. Peter Lekaneti, wakati akiwasilisha taarifa ya shughuli zilizotekelezwa na Kamati ya Kudumu ya Fedha, Utawala na Mipango kwa kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2025, kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Halmashauri, Mhe. Thomas Ngobei.
Taarifa hiyo iliwasilishwa katika Mkutano wa Pili, Kikao cha Pili cha Baraza la Tano la Madiwani kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa J.K. Nyerere, Halmashauri ya Wilaya ya Longido.
Mhe. Lekaneti alibainisha kuwa miongoni mwa mapendekezo mengine ni kuhakikisha miradi ya umaliziaji wa ujenzi wa maabara ya Shule ya Sekondari Kamwanga pamoja na madarasa ya Shule ya Msinga Kamwanga inakamilika ifikapo Februari 26, 2026.
Aliongeza kuwa gharama za ujenzi wa miradi zibainishwe kwa kuzingatia michango na nguvu za wananchi, huku Mhandisi wa Ujenzi na wataalamu wengine wa Halmashauri wakitakiwa kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi na kutoa elimu kwa jamii juu ya utunzaji wa miradi hiyo ili iweze kuleta tija.
Katika mapendekezo mengine, Mhandisi wa Ujenzi na Mkaguzi wa Ndani wametakiwa kufanya tathmini ili kubaini mbinu zilizotumika kuwezesha ukamilishaji wa miradi katika Shule ya Msingi Sinya kwa fedha zilizotolewa, ikilinganishwa na maeneo mengine ambayo miradi haikukamilika kwa kiwango kama hicho cha fedha.
Aidha, Idara ya Elimu imetakiwa kuandaa warsha kwa ajili ya Waratibu wa Elimu, Walimu Wakuu na Wakuu wa Shule ili kujifunza mbinu za ukamilishaji wa miradi kutoka kwa Mkuu wa Shule ya Msingi Sinya.
Mapendekezo mengine ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri kusimamia utolewaji wa kwa wakati wa asilimia 20 ya mapato ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyotengewa fedha katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2025/2026. Vilevile, hoja zote za ukaguzi zinazohusu malipo yasiyo na viambatanisho pamoja na risiti za EFD zimetakiwa kujibiwa na kufungwa ifikapo Februari 6, 2026.
Kadhalika, Halmashauri imetakiwa kuweka mikakati ya kushirikiana na wadau wengine katika kufuatilia marejesho ya mikopo yenye thamani ya shilingi 309,699,302 kutoka kwenye vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu.
Pia, mikakati ya kuimarisha ukusanyaji wa mapato yatokanayo na vibali vya ujenzi imependekezwa ili kufikia lengo la kukusanya shilingi milioni 11 kwa mwaka pamoja na kudhibiti ujenzi holela.
Mhe. Lekaneti ameongeza kuwa Baraza limependekeza kuongeza makisio ya mapato katika chanzo cha upimaji ardhi kutoka shilingi milioni 5 kwa mwaka, baada ya chanzo hicho kufanikiwa kukusanya kwa asilimia 200 ya makisio hadi kufikia Disemba 2025.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: +255 272 970 793/ 94
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved.