NA ABRAHAM NTAMBARA
Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, ameagiza wakuu wa shule zote wilayani humo kuhakikisha hakuna mwanafunzi anayezuiwa kuanza au kuendelea na masomo kwa sababu yoyote ile, ikiwemo kukosa sare za shule, shule zitakapofunguliwa Januari 13, 2026.
Kauli hiyo ya Mhe. Kalli imekuja siku moja baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, kutoa agizo kwa Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya pamoja na Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha hakuna mtoto anayezuiwa kuanza au kuendelea na masomo kwa sababu ya kukosa sare wakati shule zote nchini zitakapofunguliwa.
Mhe. Kalli ameyasema hayo leo Desemba 31, 2025, alipokuwa katika Shule ya Sekondari Kimokouwa wakati wa hitimisho la ziara ya siku mbili ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido, Mhe. Thomas Ngobei, ya kukagua maandalizi ya upokeaji wa wanafunzi wa Kidato cha Kwanza, Awali na Darasa la Kwanza kwa muhula wa masomo wa mwaka 2026.
Amesema kuwa amepokea rasmi agizo hilo la Waziri Prof. Shemdoe na kwamba atasimamia utekelezaji wake kwa karibu ili kuhakikisha hakuna mtoto anayekwamishwa kuanza au kuendelea na masomo pindi shule zitakapofunguliwa.
“Nimepokea agizo la Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe. Nawahakikishia wananchi kuwa hakuna mwanafunzi atakayezuiwa masomo kwa sababu ya kukosa sare. Nawaagiza walimu wakuu wasimzuie mwanafunzi yeyote kwa kigezo hicho,” amesema Mhe. Kalli.
Kutokana na agizo hilo, Mhe. Kalli amewataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanaripoti shuleni kwa wakati shule zitakapofunguliwa ili kuanza masomo bila kuchelewa.
Katika hatua nyingine, wakati akitumia fursa ya kuuaga Mwaka 2025 na kuukaribisha Mwaka Mpya wa 2026, Mhe. Kalli amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Longido.
Amesema kuwa fedha hizo zimetumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo Elimu, Maji, Afya na Barabara. Ameongeza kuwa katika mwaka 2025, shule sita zimejengwa wilayani humo, ambapo kila shule imegharimu zaidi ya shilingi milioni 580.
Aidha, amesema Wilaya ya Longido imefanikiwa kufikisha huduma ya umeme katika vijiji vyote, huku zaidi ya asilimia 84 ya vitongoji vikifikiwa na nishati ya umeme, hali inayochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa wilaya hiyo.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: +255 272 970 793/ 94
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved.