NA MWANDISHI WETU, LONGIDO
Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, amezindua rasmi zoezi la usajili na utoaji wa Bima ya Afya unaotekelezwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa awamu ya kwanza, inayohusisha wanufaika wa Mpango wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wilayani humo.
Uzinduzi huo umefanyika Februari 12, 2026 katika Ofisi ya Kata ya Longido, ambapo DC Kalli alisema kuwa jumla ya wanufaika 9,964 waliopo kwenye mpango wa TASAF wanatarajiwa kusajiliwa ma kupatiwa bima ya afya bure, gharama zote zikiwa zimelipwa na Serikali.
Alisema kuanza kwa utoaji wa bima hiyo ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyotoa wakati wa kampeni, ya kuhakikisha kuwa ndani ya siku 100 za awamu mpya ya uongozi wake, kila Mtanzania anakuwa na Bima ya Afya kupitia Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.
“Leo hapa Longido, wananchi waliopo kwenye mpango wa TASAF wanaanza kujiandikisha na kupatiwa kadi za Bima ya Afya bure. Serikali tayari imewalipia gharama zote. Nawahimiza wanufaika wote kujitokeza katika vituo vilivyotengwa ili kujiandikisha na kupata bima,” alisema DC Kalli.
Alifafanua kuwa katika awamu hii ya kwanza, zoezi la usajili na utoaji wa kadi litafanyika kwa siku tano kuanzia Februari 12, 2026, na kuwasisitiza wananchi kutumia fursa hiyo ili waweze kunufaika na huduma za afya pindi utekelezaji utakapoanza rasmi.
DC Kalli alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma za afya bure kupitia vituo vyote vya kutolea huduma vilivyopatiwa usajili nchini mara tu bima hiyo itakapoanza kufanya kazi kikamilifu.
Awali, Januari 23, 2026, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, alitangaza rasmi kuanza kwa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote kwa awamu ya kwanza, inayolenga makundi maalum yasiyo na uwezo wakiwemo wazee, watoto, wajawazito na watu wenye ulemavu, ambapo gharama zao zote zitalipiwa na Serikali.
Katika tangazo hilo, Waziri Mchengerwa pia alieleza kuwa kifurushi cha huduma muhimu kitapatikana kwa gharama ya Shilingi 150,000 kwa kaya isiyozidi watu sita chini ya skimu za Bima ya Afya.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: +255 272 970 793/ 94
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved.